MSIMU tofauti, lakini shetani yuleyule. Wakati Arsenal iliathiriwa sana na majeruhi msimu uliopita, msimu huu hadithi inaweza kuwa ileile. Kiungo wao mahiri, roho ya timu kwa sasa, Aaron Ramsey anaweza kulikosa pambano dhidi ya Man City keshokutwa kwa kuwa ni majeruhi.
Ramsey, 23, aliumia kifundo cha mguu wake katika
pambano kati ya timu yake ya taifa, Wales dhidi ya Andorra juzi ambalo
timu yake ilishinda mabao 2-1 yote yakifungwa na staa wa Real Madrid,
Gareth Bale.
Katika dakika ya 89 ya mchezo staa huyo alitolewa
uwanjani na jana alitazamiwa kupimwa kama angeweza kucheza katika
pambano dhidi ya Manchester City linalotazamiwa kuchezwa Jumamosi
mchana.
“Aaron aligongwa kidogo mguuni na akajikunja
vibaya katika kifundo cha mguu. Ilikuwa mwishoni mwa mechi na hakukuwa
na maana tena kuendelea kumchezesha. Ni matumaini atakuwa tayari kwa
ajili ya Arsenal mwishoni mwa wiki, lakini itabidi tumtazame katika saa
24 au 48 zijazo,” alisema kocha wa Wales, Chris Coleman.
Kama alivyoanza katika msimu uliopita, msimu huu
tayari Ramsey ameuanza kwa kuwa fomu akifunga mabao mawili katika mechi
tatu za Ligi Kuu ya England na alikuwa silaha kubwa kwa timu yake ya
Wales katika pambano la juzi licha ya mabao kufungwa na Bale.
Msimu uliopita, Arsenal ilikosa kasi baada ya
kuumia kwa Ramsey ambaye alikuwa katika fomu na kama akikosekana tena
kocha Arsene Wenger atakuwa katika wakati mgumu wakati huu akisaka taji
la Ligi Kuu ya England kwa mara ya kwanza tangu mwaka 2004.
Kama vile haitoshi kuna wasiwasi kuwa huenda
Arsenal pia ikamkosa staa mwingine, Mesut Ozil ambaye aliumia katika
pambano la mwisho la Arsenal dhidi ya Leicester City na alikosa mechi ya
kufuzu michuano ya Euro 2016 dhidi ya Scotland ambayo Ujerumani
ilishinda magoli 2-1.
Baada ya pambano gumu dhidi ya Man City katika
Uwanja wa Emirates Jumamosi, Arsenal watasafiri mpaka Ujerumani kwa
ajili ya kucheza pambano la kwanza la makundi ya Ligi ya Mabingwa wa
Ulaya dhidi ya Borussia Dortmund.
0 comments:
Post a Comment